HabariMazingira

KENYA YAUNGANA NA ULIMWENGU KUADHIMISHA SIKU YA BAHARI

Huku ulimwengu ukiadhimisha siku ya bahari duniani, shirika la uhifadhi wanyama Pori na viumbe majini KWS katika eneo la Kisite Mpunguti huko Lungalunga kaunti ya Kwale, limepokea boti na vifaa mbali mbali kutoka kwa shirika la uhifadhi wa mazingira nchini WWF, vitakavyo wasaidia kuzamia baharini ili kulinda na kuhifadhi viumbe majini.
Mradi wa Biopam umetoa mafunzo Kwa wavuvi na wadau wanaohusika katika uhifadhi wa mazingira ya baharini, hii ikilenga kuimarisha uchumi samawati Nchini.

Mohamed Aweri ambaye ni mkurugenzi kutoka shirika la WWF akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo vya baharini amedokeza kuwa marufuku ya utumizi wa plastic nchini umepunguza kiwango cha uchafuzi wa mazingira baharini.

Aidha amewataka Wenyeji hususan wanaoishi pambizoni mwa bahari kusitisha utumizi wa plastiki hasa katika fukwe za baharini ili kulinda matumbawe,mikoko na nyasi za baharini zinazotumika kama mazalio ya samaki.

Hayo yanajiri wakati ulimwengu ukiadhimisha siku ya bahari ulimwengu asilimia 40 ya bahari ikiwa imachafuliwa kimazingira.

>> News Desk