HabariLifestyleNews

Wafanyakazi wa Viwanja vya Ndege Wasitisha Mgomo, baada ya Maafikiano na Serikali  

Hatimaye chama cha Wafanyakazi wa Mamlaka ya Safari za Ndege nchini, KAWU kimesitisha mgomo wa wafanyakazi wa viwanja vya ndege baada ya maafikiano na Serikali.

Mgomo huo ulioanza usiku wa kuamkia Jumatano ulidumu kwa siku nzima na kusababisha kukwama kwa shughuli za safari za ndege JKIA jijni Nairobi, uwanja wa Moi mjini Mombasa, Eldoret na Kisumu.

Hii ni baada ya kikao cha kufanyika kati ya upande wa Serikali ukiongozwa na Waziri wa Uchukuzi nchini, Davis Chirchir na Katibu Mkuu wa COTU Francis Atwoli pamoja na Katibu Mkuu wa wafanyakazi hao Moses Ndiema.

Wakihutubia wafanyakazi hao uwanjani JKIA kuwaeleza yaliyokubaliwa hata hivyo Waziri Chirchir alikuwa na wakati mgumu kujieleza baada ya wafanyakazi hao kuendelea kushinikiza kutoruhusiwa kampuni ya Adani kuchukua jukumu la kusimamia uwanja huo.

Waziri Chirchir akiendelea kutetea hatua ya Serikali ya kuukabidhi uwanja huo kwa kampuni ya Adani.

Akisoma yale waliokubaliana na kusitishwa kwa mgomo huo, Katibu Mkuu wa chama cha kutetea maslahi ya Wafanyakazi nchini, COTU Francis Atwoli amesema hakutakuwa na mfanyakazi yeyote atakayewajibishwa kutokana na mgomo huo na kwamba maslahi yao yatashughulikiwa vilivyo.

Katika makubaliano hayo aidha Kaimu Mkurugenzi wa KAA Henry Ocoye ametakiwa kujadiliana na kuhakikiahs mawasilianao mwafaka na ofisi ya chama cha wafanyakazi wa uwanja wa ndege, KAWU.

Hata hivyo kwa upande wake Katibu Mkuu wa chama cha Wafanyakazi wa viwaja vya ndege, Moses Ndiema amesema licha ya kusitisha mgomo huo hawaijakubali kampuni ya Adani, lakini watakuwa na sauti katika hatua yoyote itakayochukuliwa kabla kuafikia uamuzi wowote wa baadaye.

By Mjomba Rashid