HabariSiasa

Kembi Gitura atimuliwa kama mwenyekiti wa bodi ya KEMSA……..

Rais Uhuru Kenyatta amemteua Marry Chao Mwadime kuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa mamlaka ya kusambaza dawa nchini KEMSA kwa kipindi cha miaka 3.

Katika ilani ya gazeti rasmi la serikali, rais amebatilisha uteuzi wa KEMBI Gitura kama mwenyekiti wa bodi hiyo.

Katika ilani hiyo, waziri wa afya Mutahi Kagwe amewateua Lawrence Wahome, Robert Nyarango, Terry Kiunge Ramadhani na Lincoln Nyaga kama wanachama wa bodi hiyo ya wakurugenzi kwa muda wa miaka 3.

Mwezi uliopita, wabunge walielezea wasiwasi kuhusu uteuzi wa Gitura kwa Mamlaka ya Mawasiliano.

Kamati ya bunge chini ya uwenyekiti wa mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir ilisema uteuzi wa seneta huyo wa zamani wa Murang’a haufanywa kwa nia nzuri ikizingatiwa uchunguzi wa kashfa ya Kemsa unaoendelea.

Ikumbukwe wiki iliyopita Gitura alichaguliwa kuhudumu katika mamlaka ya mawasiliano nchini CA.

Hatua hii inajiri wakati mamlaka ya KEMSA imekuwa ikishutumiwa vikali kwa madai ya ufisadi, haswa kuhusu matumizi ya fedha zilizotengwa kukabili maambukizi ya corona.

kwa sasa uchunguzi dhidi ya mamlaka hiyo unaendelea huku kamati ya bunge kuhusu uwekezaji ikiendelea kuwahoji watu kadhaa wakiwemo maafisa wa KEMSA na wakuu wa kampuni zilizopewa zabuni ya kusambaza vifaa vya matibabu.

Sakati hiyo ya KEMSA pia inadaiwa kusababisha mvutano baina ya serikali na shirika ala USAID kuhusu usambazaji wa dawa za kukabili makali ya virusi vya HIV.

 

By: Warda Ahmed