HabariNewsUncategorized

Hatma ya Mazungumzo ya maridhiano i mashakani; Azimio ikitishia kutokubali ripoti

Hatma ya Mazungumzo ya maridhiano i m

Ati ati na kitendawili kinagubika hatma ya ripoti ya mazungumzo ya maridhiano baada ya Mrengo wa Azimio la Umoja One Kenya kutishia kutotia saini endapo maswala makuu yanayoshinikizwa na mrengo huo hayatazingatiwa.

Kiongozi wa Azimio Raila Odinga ameorodhesha swala la kupanda kwa gharama ya maisha, kuundwa upwa kwa Tume ya Uchaguzi na Mipaka, IEBC, ukaguzi wa sava za IEBC, kutoingilia vyama vingine vya kisiasa pamoja na kupunguzwa kwa ushuru katika bidhaa za mafuta kuwa masuala muhimu yanayostahili kuangaziwa.

Kupitia kwa taarifa vyombo vya habari Alhamisi, Odinga alisema hapatakuwepo na ushirikiano baina ya Upinzani na Serikali iwapo masuala hayo hayatapewa kipau mbele kwani ni masuala yanayomuathiri mwananchi wa kawaida.

“Tumesema gharama ya maisha mpaka irudi chini, ingine ni kuundwa kwa Tume ya Uchaguzi, tatu ni ukaguzi wa matokeo ya uchaguzi uliopita, nne ni mambo ya kutoingiliwa kwa vyama vingine vya kisiasa lakini muhimu zaidi ni gharama ya maisha lazima irudi chini.” Alisema.

Ile ushuru waliweka kwa mafuta itolewe kutoka asilimia 16 irudishwe kule ilikuwako asilimia 8, kama hawawezi kukubali hiyo tunasema hakuna mazungumzo hakuna maafikiano,” alikariri Odinga

Katika kikao tofauti Kinara wa Chama cha Narc Kenya Martha Karua amesema kwamba Azimio itaregelea maandamano iwapo mazungumzo yatagonga mwamba huku akisisitiza kwamba ni lazima Serikali kutilia maanani masuala yote yanayoibuliwa na Azimio.

Mazungumzo ambayo wanaelekea kumalizia kama Azimio tulitoa mambo 3 muhimu pia; gharama ya maisha, haki za uchaguzi ambayo wafungue sava na suala la tatu heshima kwa vyama vya kisiasa,” alisema Karua.

Tunataka kusema suala la gharama ya maisha si suala la unga pekee, japo unga ni muhimu sana lakini suala la elimu ya bure ya msingi na sekondari inahujumiwa na watoto wengi wanakosa shule, tunataka kuona ufadhili wa elimu ya vyuo vikuu unarejeshwa pale ulikuwa, mikopo ya wanafunzi wa vyuo sharti ipewe wote na sio kwa wachache tu,” alisisitiza Karua.

Vilevile Karua alibaini kwamba gharama ya juu ya maisha si bei ya unga pekee bali Elimu ya msingi na sekondari bila malipo, bei ya mafuta kupunguzwa na ada ya vyuo vikuu kukadiriwa.

Wakati uo huo Odinga aliitaka Serikali kufutilia mbali mkataba wa ununuzi wa mafuta baina yake na mataifa ya Arabuni.

Katika kikao na waandishi wa Habari mapema Alhamisi, kwenye Wakfu wa Jaramogi Oginga Odinga, Kinara huyo wa Azimio aliutaja mkataba huo wa kununua mafuta kutoka serika kwa serikali (G2G) kuwa wa ulaghai mkubwa.

Alibainisha wazi kwamba mkataba huo uliotiwa saini unanuia kupandisha gharama ya mafuta nchini zaidi na kufaidisha baadhi ya viongozi wakuu serikalini aliowataja kuwa matapeli.

BY MJOMBA RASHID