HabariNews

Mbwe Mbwe za Mtihani zashuhudiwa Wanafunzi Wakisherehekea Matokeo ya KCPE Kilifi

Mbwe mbwe zinaendelea kushuhudiwa siku moja baada ya kutangazwa rasmi kwa matokeo ya mtihani wa kitaifa KCPE, huku shule ya Elite Academy, Shariani, kaunti ya Kilifi ikitia fora kwenye mitihani hiyo.

Sherehe za aina yake zikiendelea kushuhudiwa kaunti ya Kilifi kufuatia kutangazwa kwa matokeo ya mitahani wa kitaifa KCPE, shule ya Mtwapa Elite Academy Shariani, ikiwa ya hivi karibuni kuonesha ubabe wake kwenye mtihani huo kwa kuandikisha matokeo bora mwaka huu.

Kwa mujibu wa mwalimu mkuu wa shule hiyo Fred Okoth ushirikiano baina ya walimu, wazazi na wanafunzi ndicho chanzo kikuu cha wao kuandikisha matokeo hayo bora.

Aliwasihi wazazi kuwatia moyo watoto wao na kukubali matokeo waliyopata ili kuwaepusha kujidhuru pamoja na kuwasabishia matatizo ya afya ya akili.

Kwa upande wake Loyce Nyale mwanafunzi bora katika shule hiyo kwa kupata alama 414 ameelezea furaha yake huku akipongeza juhudi za walimu na wanafunzi wenzake, akisema kuwa zimechangia kumfikisha yeye kwenye mafanikio hayo.

….

Eliud Nyale aliyepata alama 407 alisema kuwa bidii katika masomo yake imemfanikisha kwenye mtihani huo huku akielezea azma yake ya kuwa mhandisi.

Kwenye matokeo mengine Bradley Mtalii Thoya, mwanafunzi katika shule ya msingi ya Galilee Roka, eneo bunge la Kilifi Kaskazini amefanikiwa kupata alama 417 na kuwa mwanafunzi bora shuleni humo.

BY ERICKSON KADZEHA