HabariLifestyleMazingiraMombasaNews

–Utepetevu Wa Wazazi Katika Malezi Wachangia Ongezeko La Utumizi Wa Mihadarati Pwani.

Utepetevu wa wazazi na Malezi mabaya kwa watoto yametajwa kuchangia pakubwa katika ongezeko la utumizi wa mihadarati nchini hasa eneo la Pwani.

Mkurugenzi wa mamalaka ya kitaifa ya kupambana na utumizi wa pombe na mihadarati ukanda wa Pwani, NACADA, George Karisa alisema wazazi wengi wamekosa kuzingatia maadili na jukumu la malezi bora kwa wana wao na kusahau kuwa kielelezo na mfano wa bora wa kuigwa kwa watoto na badala yake.

Katika mahojiano ya Kipekee na Meza yetu ya Habari mnamo siku ya Alhamisi  Karisa alibaini kuwa mandhari ya mwambao na upatikanaji wa mihdarati kwa urahisi, ushawishi kutoka kwa watumizi na ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana zingali changamoto kuu katika vita dhidi ya utumizi wa mihadarati.

“Kuna swala moja ambalo linajitokeza ambalo watu hawaliangazii swala malezi mabaya ambalo limechangia vijana wengi kujiingiza katika uraibu ,kama mazazi unafaa kuwa mfano bora lakini wewe unakula miraa unatarajia nini kutoka kwa mtoto,hizi dawa zinapatikana kiurahisi,vijana wengi wanashawishika hawana kazi.” Alisema Karisa.

Wakati huo huo Karisa alisema kuwa mandhari ya mwambao wa Pwani kuwa na vivutio vya utalii kumepelekea kuwepo mianya mingi inayotumika kuingiza mihadarati na kuchangia ongezeko la utumizi wa mihadarati katika ukanda huu.

“Hapa Pwani vile tulivyo tunasema kuwa inachangia kwa sababu ya kuna mianyaa ambayo watu wanaweza kuingia kiurahisi hakuna ulinzi wa kutosha kwa hivyo hio hali bado ni changamoto.” Alisema Karisa.

Ikumbukwe kuwa kulingana na ripoti ya utafiti wa NACADA mwaka 2022 imeonyesha Pwani inaongoza takwimu za kitaifa kwa kuwa na asilimia kubwa ya watu waliotumia japo aina moja ya mihadarati.

Haya yanajiri huku NACADA ikiendeleza kampeini ya uhamasisho kuhusu mihadarati, ambapo taifa linaadhimisha Wiki ya Kitaifa ya Kuzuia utumizi wa mihadarati.

BY MEDZA MDOE