Mahakama ya Shanzu mjini Mombasa iliamuru kuzuiliwa kwa mhubiri tata Paul Makenzie na washirika wake 27 kwa siku saba zaidi wanaoshukiwa na mauaji ya halaiki kwenye msitu wa Shakahola Kaunti ya Kilifi.
Upande wa mashtaka kupitia kwa Naibu Mkuu wa Mashtaka ya Umma DPP ulisisitiza kuwa ombi la kuzuiliwa kwa miezi sita zaidi kwa washukiwa hao ni halali kwa kuzingatia uzito wa kesi hiyo.
Mahakama hata hivyo ilisema kuwa uamuzi zaidi utatolewa tarehe 19 Oktoba kuhusu ombi la kuzuiliwa kwa washukiwa hao kwa miezi 6 huku uchunguzi zaidi ukiendelea.
Kwa upande wake wakili wa utetezi Wycliffe Makasembo alipinga ombi hilo akisema kwamba kuendelea kuzuiliwa kwa wateja wake ni kukiuka haki zao kama watuhumiwa.
Mackenzie na wafuasi wenza wanakumbwa na mashtaka yasiyopungua 12 ikiwemo mauaji, ushauri uliosababisha watu kujitoa uhai utekaji nyara na ukatili kwa watoto.