HabariNews

Simba Mla watu Kwale auawa; Wakazi watakiwa kuendelea kuwa Waangalifu

Hatimaye simba mla watu aliyemwua kijana mmoja mhudumu wa bodaboda kaunti ya Kwale wiki

moja iliyopita amekamatwa na kuuawa.

Simba huyo amelazimika kuuawa kwa mujibu wa kanuni na desturi ya shirika la wanyamapori nchini, KWS.

Akithibitisha taarifa hiyo wakati wa mahojiano na kituo kimoja cha habari hapa Pwani Naibu Msemaji wa

Serikali Mwanaisha Chidzuga amesema kuwa tayari simba huyo ameuawa na sasa wenyeji wapo huru

kuendeleza shughuli zao pasi na uoga.

 

Hata hivyo kiongozi huyo amewataka wenyeji hao kuchukua tahadhari kabla ya hatari na kuwa waangalifu

zaidi nyakati za usiku ili kuepukana uvamizi wa wanyamapori wengine hatari. “Yule simba mla watu ameweza

kukamatwa na kuuliwa, unajua katika desturi ya Wanyamapori KWS simba akiua watu lazima auawe, huwa

ashaonja damu so lazima auawe asiwe kwenye mbuga, ni salama zaidi. Tunawaambia wakazi watoe hofu lakini

tunawasihi waendelee kuwa waangalifu zaidi maana kuna ndovu na kuna nyoka, vyema wajihadhari, so if you

can waepuke kutumia barabara zile nyakati za usiku,” alisema.

 

Simba huyo mla watu alidaiwa kumshambulia na kumwua mhudumu mmoja wa bodaboda eneo la Marere katika

barabara ya Kwale-Kinango, ambapo mwili wa jamaa huyo ulipatikana kando ya pikipiki hiyo ukiwa umeliwa

sehemu za tumboni na chini.

BY DAVID OTIENO